
Ndoa iliyo bora na furaha tele haianzi hewani bali
ina msingi wake. Furaha siyo kitu cha kupata kama bahati nasibu. Ni jambo
ambalo unajenga kama mtu ajengavyo nyumba imara. Lazima aweke msingi ambao
utafanya nyumba idumu au ianguke. Hivyo kijana wa kiume na wa kike picha halisi
ya ndoa bora na yenye amani inafanyika wakati wa uchaguzi wako wa kupata mwenzi
wa maisha yako. Uchaguzi wowote na namna ulivyofanyika utaamua hatima ya aina
ya ndoa uitakayo. Zipo kanuni chache tutakazoziangalia kwa vijana wa kike na
kiume namna wanavyoweza kupata mwenzi atakayewapa furaha na amani tele katika
nyumba zao badala ya majuto na huzuni. Na pia kuondoa kauli laiti ningejua au
najuta kuolewa na mwanaume huyu ama kumuoa mwanamke huyu.
MVULANA
UTAMPATAJE MSICHANA ATAKAYEKUWA MWENZI ANAYEFAA
Zipo
kanuni za msingi ambazo kama kijana wa kiume unaweza kufanya katika uchaguzi
wako. Hebu twende hatua kwa hatua katika swala hili:
- Kijana mpatie Yesu maisha yako kwa
asilimia 100. Jitoe kwa Yesu ili akupe mke mwema. Kumbuka mke mwema hutoka
kwa Bwana. MITHALI 31:10.
- Maombi ndio silaha na dira
itakayokuonyesha chaguo lako. Orodhesha sifa za binti umtakaye awe mwenzi
wako. Huenda awe msomi, mfanyakazi, mkulima, mtu wa kiroho, mkarimu, na
kadhalika. MWANZO Kisa cha Isaka na Rebeka.
- Fanya uchaguzi wa mchumba. Kisha
anza kujenga urafiki na pia fanya uchunguzi wa mwenendo wa maisha yake ili
upate dalili uzitakazo. Hapa usiharikishe kumtakia kuwa utamuoa maana
ataficha makucha yake.
- Fanya liwe ni jambo la lazima
kuoana na mtu wa imani moja na wewe. Usikubali kuoana na mtu ambaye siyo
wa imani moja na wewe. Mkatoliki awe mkatoliki. Mwislamu hali kadhalika.
Epuka kugawa watoto na kuondoa furaha na umoja wa familia. Na hata
kushindana katika mambo ya imani.
- Chukua muda wa kutosha kujifunza tabia
yake. Usiharakishe kumuoa bila kujifunza tabia yake. Uchumba wenu
usipungue miezi sita na kuendelea. Upande wa pili usizidi sana miaka
minne. Muda mfupi haukupatia nafasi ya kujua madhaifu yake na mazuri yake.
Muda mrefu nao unaleta mashaka na kujaribiwa kwa mwenzi wako anapoona
miaka inasonga hasa mwanamke.
- Oana na mwanamke ambaye tabia zenu
zinafanana ama kulingana au kuendana. Kama ni mkulima basi usitafute binti
wa ofisini yatakushinda.
- Kijana epuka kuoa maumbile ya
mwanamke (physical appearance). Wengi wanajutia kwani hakujua mwili huwa
unachujuka wakati mwanamke anapoolewa aidha kwa kuzaa ama kukabaliana na
changamoto za ndoa. Miguu ya bia huwa inabadilika na kuwa ya Coca Cola.
Namba nane huwa namba moja.
- Usifanye uchaguzi wa sura pekee
kama kiini cha chaguo lake. Bali tabia iwe ndicho kiini cha kwanza na sura
iwe namba pili. Ni kweli ni vizuri ukaoa mwanamke ambaye ana sura nzuri
hata ukitembea barabara unafahari kwenda naye. Siyo ambaye unaona haya
kumtambulisha kama mkeo. Lakini sura ikiwa ndicho kiini utaishia kwenye
majuta kila siku maana visura wengi bado hawajazaliwa.
- Unapopata msichana tafuta ushauri
wa watu wenye heshima wanaomfahamu vizuri. Wanaweza kuwa wachungaji,
masheikh, wazee au watu wa makamo.
- Epuka msichana mwenye tamaa vitu.
Msichana anayekuomba mara hiki au kile huyo atakusumbua mapema.
- Jaribu kujua habari za marafiki wa
karibu sana wa Yule msichana. Utakapoona na wale ambao hapo mtaani
wanasifika kwa tabia mbaya ni dalili mbaya kwa mahusiano yako na yake.
Hapa unaweza kumpima kwa kutoka naye out’utakapoona anasimamishwa kila
kona tambua kuwa huyo ni jamvi la wageni. Msichana anayejiheshimu huwezi
kusimamishwa njia yote na wanaume.
- Mwisho: Unapogundua mapungufu
ambayo huyapendi ni bora kuvunja uchumba kuliko kuvunja ndoa. Tambua
huwezi kumbadilisha mtu tabia yake. JASIRI HAACHI ASILI!
MSICHANA UTAPATAJE
MVULANA ANAYEKUFAA MAISHANI MWAKO
Kazi
ya ziada kwa msichana kujua mvulana ambaye ni wa kweli. Kwani ni vigumu sana
kwa wasichana wengi kujifunza tabia ya kijana wa kiume kwa makini sana.
Wasichana wanaona haya kuuliza habari za mvulana Fulani kwa watu kwani
wanaogopwa kuulizwa unataka nini kwake. Lakini yapo mambo ya muhimu sana ambayo
msichana unaweza kufanya ili kupata mwenzi ambaye atakupa furaha ya kweli
katika ndoa yako. Kumbuka mwanamke nawe unauchaguzi wa kufanya. Fanya mambo
yafuatayo:
- Msichana jitoe maisha yako kwa Yesu
kwa asilimia zote ili Bwana akupatie kilicho bora maishani mwako. MITHALI 16:7
- Msichana jiheshimu sana mbele za
watu na hata uwe mwaminifu mbele ya jamii unayoishi.
- Weka swala hili katika maombi na
pia weka sifa Fulani ambazo unazitaka kutoka kwa Mungu kwa mwenzi
atakayekupatia. Sifa ya kwanza ombea upate mcha Mungu.
- Usikatishwe tamaa unapoona vijana
wengi hawakufuati. Tulia maana siku zote mambo mazuri hayana haraka.
Usipayuke yuke kuwa mbona huolewi.
- Chagua mwanaume anayependa kazi.
Usibague kazi anayofanya alimradi ni mtu mwenye bidii acha kuangalia uzuri
wa kazi yake. Mwenye bidii anaweza kubadilisha maisha katika hali yeyote
wakati wowote.
- Usikubali kwa gharama iwayo yote
kuolewa na mtu ambaye hapendi kazi. Epuka kugeuzwe kuwa kiwanda cha watoto
na kuzalishia mali. Epuka kulala njaa na watoto. Ukiolewa na mvuvi nyumba
yake itakuwa na taabu nyingi na umasikini mwingi.
- Jenga urafiki na wavulana wote kwa
heshima. Usibague wavulana wa kuzungumza nao. Wanaume wengi wanaogopwa
kudharauliwa na kuaibishwa na wanawake.
- Epuka kama ukoma kuolewa mtu
asiyeamini au mtu asiye wa imani moja na wewe. Ni vigumu sana kwa wanaume
kubadilisha dini yake.
- Olewa na mtu mnayefanana tabia
zenu. Kama ni mlevi basi olewa na mlevi mwenzako au mvuta sigara mwenzake
ili starehe ya mwingine isiwe kero
ya mwingine. Ijapokuwa nyumba ya mlevi kumbuka haina amani. MITHALI 20:1; 23:30 – 35.
- Msichana inakupasa uwe ni mtu wa
gharama kubwa. Jiweke katika kiwango cha juu hata kama unatoka katika
familia masikini. Usikubali kupewa zawadi ovyo ovyo. Kumbuka kila zawadi
inayotolewa na mwanaume utailipa.
- Usikubali kuolewa na mali au fedha
au umaarufu wa mtu. Kumbuka ikiwa utakuwa umefuata hivyo vitu huwa
vinayeyuka na matokeo yake upendo wako utayeyuka pia maana ndivyo
ulivyofuata hapo. Ni bora kuolewa na masikini anayempenda Mungu kuliko
tajiri ambaye hana hofu ya Mungu atakuletea wanawake wengine.
- Msichana ni sumu kwa kufanya mapenzi
na mvulana unayetaka awe mume wako. Jambo hili litaondoa uaminifu katika
ndoa yako na kisha kutakuwa na tabia ya kutokuaminiana siku zote. Ikiwa
anakuambia mpaka mfanye kitendo hicho ndipo akuoe ni bora ukavunja uchumba
maana kijana huyo sio Mwaminifu kabisa.
No comments:
Post a Comment