Pages

IMANI ZA MSINGI ZA WAADVENTISTA WASABATO



1.       Maandiko Matakatifu

Maandiko Matakatifu yaani Agano la Kale na Jipya ndiyo neno la Mungu lililoandikwa likatolewa kwa uvuvio wa Mungu, kupitia kwa watu watakatifu wa Mungu walionena na kuandika kama walivyoongozwa na Roho Mtakatifu. Ndani ya Neno hili, Mungu amemkabidhi mwanadamu maarifa yaliyo lazima kwa ajili ya wokovu. Maandiko Matakatifu ni ufunuo usioweza kukosa wa mapenzi yake. Ndiyo upeo wa tabia, kipimo cha uzoefu, ufunuo thabiti wenye mamlaka wa mafundisho ya imani, na kumbukumbu aminifu ya matendo ya Mungu katika historia. (IIPet.1:20, 21; IITim. 3:16, 17: Zab. 119:105l Mith. 30:5, 6; Isa. 8:20; Yoh. 17:17; IWathe. 2:13; Waeb. 4:12)

2.      Utatu Mtakatifu

Kuna Mungu mmoja: Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu, umoja wa Nafsi tatu za milele. Mungu hapatikani na mauti, mwenye nguvu zote, ajuaye yote, zaidi ya yote, na aliyeko daima. Yeye hana mwisho na ni zaidi ya ufahamu wa kibinadamu, hata hivyo anafahamika kupitia kujifunua kwake Binafsi. Milele zote yu astahili kuabudiwa, kusujudiwa, na viumbe wote. (Kumb. 6:4; Mathayo 28:19; IIWakor. 13:14; Waef. 4:4-6; IIPet. 1:2; Itim. 1:17; Ufnl 14:7)

3.      Baba

Mungu Baba wa milele ndiye Muumbaji, chimbuko, Mtegemezaji, na Mfalme wa viumbe wote. Ni mwenye haki na Mtakatifu, mwingi wa rehema, mwenye fadhili, si mwepesi wa hsira, ni mwingi wa uthabiti wa upendo na uaminifu. Tabia na uwezo vilivyodhihirishwa ndani ya Mwana na Roho Mtakatifu pia ni ufunuo wa Baba. (Mwa. 1:1; Ufun. 4:11; IWakor. 15:28; Yoh. 3:16; IYoh. 4:8; ITim. 1:17; Kut. 34:6, 7; Yoh. 14:9).

4.                  Mwana

Mungu Mwana wa milele alifanyika mwili katika Yesu Kristo. Kupitia kwake vitu vyote viliumbwa, tabia ya Mungu imefunuliwa, wokovu wa wanadamu unakamilishwa na ulimwengu unahukumiwa. Milele zote Mungu kweli, Alifanyika mwanadamu kweli, Yesu aliye Kristo. Alichukuliwa mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu na kuzaliwa na bikira Mariamu. Akaishi na kupitia uzoefu wa majaribu kama mwanadamu, lakini kwa ukamilifu alionyesha kwa mfano haki na upendo wa Mungu. Kwa miujiza yake alidhihirisha uwezo wa Mungu na alithibitishwa kama Masihi aliyeahidiwa. Aliteseka na kufa kwa hiari msalabani kwa ajili ya dhambi zetu, na kuhudumu katika hekalu la mbinguni kwa niaba yetu. Atakuja tena katika utukufu kwa ajili ya ukombozi wa mwisho wa watu wake na urejeshwaji wa vitu vyote. (Yoh. 1:1 – 3, 14; Wakol. 1:15 – 19; Yoh. 10:30; Wafil. 2:5 – 11; Waebr. 2:9 – 18; IWakor. 15:3, 4; Waebr. 8:1, 2; Yoh. 14:9; Warumi 6:23: IIWakor. 5:17 – 19; Luka 1:35; Yoh. 14:1 – 3)

5.                  Roho Mtakatifu

Mungu Roho wa milele alikuwa mtendaji pamoja na Baba na Mwana katika uumbaji, kufanyika mwili, na katika ukombozi. Aliwavuvia waandishi wa Maandiko Matakatifu, alijaza maisha ya Kristo na uwezo. Huwavuta na kuwasadikisha wanadamu; na wale wanaoitikia huwafanya upya na kuwabadilisha katika sura ya Mungu. Akipelekwa na Baba na Mwana ili kuwa siku zote pamoja na watoto wake, hutoa karama za kiroho kwa kanisa, huliwezesha kumshuhudia Kristo, na kwa upatano na Maandiko huliongoza kwenye ukweli wote. (Mwa. 1:2; Luka 1:35; 4:18; Mdo. 10:38; IIPet. 1:21; IIWakor. 3:18; Waef. 4:11, 12; Mdo. 1:8; Yoh. 14:16 – 18, 26; 15:26, 27; 16:7 – 13)

6.                  Uumbaji

Mungu ni Muumba wa vitu vyote, na amefunua katika Maandiko uhalisi wa tukio la shughuli zake za uumbaji. Katika siku sita Bwana alizifanya “mbingu na nchi” na vitu vyote vilivyo hai juu ya nchi, akastarehe siku ya saba ya juma lile la kwanza. Na hivyo akaanzisha Sabato kama kumbukumbu ya milele ya kukamilika kwa kazi yake ya uumbaji. Mwanamume na mwanamke wa kwanza walifanywa kwa mfano wa Mungu kama upeo wa kazi yake ya uumbaji, wakapewa utawala juu ya ulimwengu, na wakaagizwa kuwajibika na utunzaji wake. Wakati ulimwengu ulipomalizika kila kitu kilikuwa “ni chema sana,” ukitangaza utukufu wa Mungu. (Mwa. 1:2; Kut. 20:8 – 11; Zab. 19:1 – 6; 33:6, 9; Waeb11:3)

7.                  Asili ya Mwanadamu

Mwanamume na Mwanamke walifanywa kwa mfano wa Mungu wakiwa kila mmoja na nafsi yake, uwezo na uhuru wa kufikiri na kutenda. Ingawa waliumbwa viumbe huru, kila mmoja ni umoja wa nafsi isiyogawanyika ya mwili, akili na roho, akimtegemea Mungu kwa uhai na pumzi na mengine yote. Wakati wazazi wetu wa kwanza walipomwasi Mungu, walikana utegemezi wao kwa Mungu na wakaanguka kutoka hadhi yao ya juu chini ya Mungu. Sura ya Mungu iliyokuwa ndani yao iliharibiwa na wakawa chini ya mauti. Wanazaliwa wakiwa na udhaifu na mivuto ya kuelekea kwenye uovu. Lakini Mungu katika Kristo alipatanisha ulimwengu na nafsi yake, na kwa njia ya Roho wake hurjesha ndani ya wnadamu watubuo sura ya Muumba wao. Wakiwa wameumbwa kwa ajili ya utukutu wa Mungu , wanaitwa kumpenda na kupendana wao wa wao, na kutunza mazingira yao. (Mwa. 1:26 – 28; 2:7; Zab. 8:4 – 8; Mtdo. 17:24 – 28; Mwa. 3; Zab. 51:5; Warumi 5:12 – 17; IIWakor. 5:19, 20; Zab. 51:10; IYoh. 4:7, 8, 11, 20; Mwa. 2:15)

8.                  Pambano Kuu

Jamii yote ya wanadamu sasa inahusika katika pambano kuu baina ya Kristo na Shetani kuhusu tabia ya Mungu, sheria yake, na utawala wake juu ya ulimwengu. Ugonvi huu ulianza mbinguni wakati kiumbe aliyeumbwa na kutunukiwa uhuru wa kuchagua, katika kujiinua akawa shetani, mpinzani wa Mungu, na kupelekea sehemu ya malaika kwenye uasi. Akaingiza roho ya uasi katika ulimwengu huu pale alipowaongoza Adamu na Hawa kuingia dhambini. Dhambi hii ya mwanadamu ilileta matokeo ya upotoshaji wa sura ya Mungu katika wanadamu, uvurugaji wa ulimwengu ulioumbwa, na mwishowe kuteketea wakati wa gharika iliyoukumba ulimwengu wote. Ukitazamwa na viumbe wote, ulimwengu huu ukawa uwanja wa vita ya ulimwengu, ambao kutokana nao Mungu wa upendo hatimaye atathibitika kuwa mwenye haki. Katika kuwasaidia watu wake katika pambano hili, Kristo anamtuma Roho Mtakatifu na malaika watiifu kuongoza, kulinda, na kutegemeza katika njia ya wokovu. (Ufun. 12:4 – 9; Isaya 14: 12 – 14; Ezek. 28:12 – 18; Mwa. 3; Warumi 1:19 – 32; 5:12 – 21; 8:19 – 22; Mwa. 6 – 8; IIPet. 3:6l IWakor. 4:9; Webr. 1:14)




9.                  Maisha, Mauti na Ufufuo wa Kristo

Katika maisha ya Kristo ya utii mkamilifu kwa mapenzi ya Mungu, mateso yake, mauti na ufufuo, Mungu alitoa njia pekee ya kafara kwa ajili ya dhambi ya mwanadamu, ili kwamba wale ambao kwa imani wanapokea upatanisho huu waweze kuelewa vizuri zaidi upendo mtakatifu usio na kikomo wa Muumbaji. Kafara hii kamilifu huthibitisha haki ya sheria ya Mungu na fadhili za tabia yake; kwa sababu hufanya vyote viwili kuhukumu dhambi yetu na kutupatia msamaha. Kifo cha Kristo ni cha badala na cha kulipia, kupatanisha na chenye kubadilisha. Ufufuo wa Kristo hutangaza ushindi wa Mungu dhidi ya nguvu za uovu, na kwa wale wanopokea kafara huhakikisha ushindi wao wa mwisho dhidi ya dhambi na mauti. Kinatangaza ukuu wa Yesu Kristo, ambaye mbele zake kila goti mbinguni na duniani litapigwa. (Yoh. 3:16; Isaya 53:1; IPet. 2:21, 22; IWakor. 15:3, 4, 20 – 22; IIWakor. 5:14, 15, 19 – 21; Warumi 1:4; 3:25; 4:25; 8:3, 4; IYoh 2:2; 4:10; Wakol. 2:15; Wafilipi 2: 6 – 11).

10.               Uzoefu na Wokovu

Katika upendo usio na mwisho na rehema zake Mungu alimfanya Kristo, asiyejua dhambi kuwa dhambi kwa ajili yetu, ili kwamba katika yeye tuweze kufanywa haki ya Mungu. Tukiongozwa na Roho Mtakatifu tunatambua hitaji letu, tunakiri hali yetu ya kuwa wenye dhambi, tunatubu maasi yetu, na kuonyesha imani katika Yesu kama Bwana Kristo, kama Mbadala na Kielelezo. Imani hii inayopokea wokovu huja kupitia katika uwezo wa kimbimgu wa Neno na ni karama ya neema ya Mungu. Kupitia kwa Kristo tunahesabiwa haki, tunafanywa kuwa wana na binti za Mungu, na kukombolewa kutoka katika hali ya kuwa chini ya dhambi. Kupitia kwa Roho tunazaliwa upya na kutakaswa; Roho hufanya upya nia zetu, huandika sheria ya Mungu ya upendo katika mioyo yetu, na tunapewa uwezo wa kuishi maisha matakatifu. Tukikaa ndani yake tunakuwa washirika wa asili ya uungu na tuna hakika ya wokovu sasa na katika hukumu. (IIWakor. 5:17 – 21; Yoh. 3:16; Wag. 1:4; 4:4 – 7; Tito 3:3 – 7; Yoh. 16:8; Wag. 3:13, 14; IPet. 2:21, 22; Warumi 10:17; Luka 17:5; Marko 9:23, 24; Waef. 2:5 – 10; Warumi 3:21 – 26; Wakol. 1:13, 14; Warumi 8:14 – 17; Wag. 3:26; Yoh. 3:3 – 8; IIPet. 1:3, 4; Warumi 8:1 – 4; 5:6 – 10)

11.               Kukua katika Kristo

Kwa kifo chake msalabani Yesu alizishinda nguvu za uovu. Yeye aliyewatiisha pepo wachafu wakati wa huduma yake hapa duniani amezivunja nguvu zao na kuthibitisha kuwa mwisho wao ni uangamivu usioepukika. Ushindi wa Yesu hutupatia ushindi dhidi ya nguvu za uovu ambazo bado zinatafuta kututawala, tunapotembea naye kwa imani, furaha, na uhakika wa upendo wake. Sasa Roho Mtakatifu anakaa ndani yetu na kututia nguvu. Tukidumu kujikabidhi kwa Yesu kama Bwana na Mwokozi wetu tunawekwa huru kutoka katika mzigo wa matendo yetu yaliyopita. Hatuishi tena gizani, katika hofu ya nguvu za uovu, ujinga, na katika kukosa maana kwa namna ya maisha yetu ya awali. Katika uhuru huu mpya ndani ya Kristo, tumeitwa kukua katika kufanana na tabia yake, tukiongea naye kila siku katika sala, na kujilisha neno lake, tukilitafakari neno lake na majaaliwa yake, tukiimba sifa zake, tukikusanyika pamoja kwa ajili ya ibada, a kushiriki katika utume wa kanisa. Tukijitoa katika kuwahudumia kwa upendo wale wanaotuzunguka na katika kuwashuhudia wokovu wake, kuwepo kwake nasi daima kwa njia ya Roho hugeuza kila wasaa na kila kazi kuwa uzoefu wa kiroho. (Zab. 1:1, 2; 23:4; 77:11, 12; Kol. 1:13, 14; 2:6, 14, 15; Luka 10:17 – 20; Efeso 5:19, 20; 6:12 – 18; IThes. 5:23; IIPet. 2:9; 3:18; IIWakor. 3:17, 18; Filipi 3:7 – 14; IThes, 5:16 – 18; Math. 20:25 – 28; Yoh. 20:21; Gal. 5:22 – 25; Warumi 8:38, 39; IYoh. 4:4; Waebr. 10:25.)


12.               Kanisa

Kanisa ni jamii ya waumini wanaimkiri Yesu Kristo kuwa Bwana na Mwokozi wao. Katika kufungamana na watu wa Mungu katika nyakati za Agano la kale, tunaitwa kutoka katika ulimwengu; na tunajiunga pamoja kwa ajili ya huduma kwa wanadamu wote, na kwa ajili ya tangazo la injili ulimwenguni mwote. Kanisa linapata mamlaka yake kutoka kwa Kristo, aliye Neno lililofanyika mwili, na kutoka katika Maandiko, ambayo ndiyo Neno lililoandikwa. Kanisa ni jamaa ya Mungu; waliofanywa na Yeye kuwa watoto wake, washiriki wake huishi katika msingi wa agano jipya. Kanisa ni mwili wa Kristo, jamii ya wale wenye imani ambayo Kristo mwenyewe ndiye kichwa. Kanisa ni bibi arusi ambaye kwa ajili yake Kristo alikufa ili apate kulitakasa na kulisafisha. Wakati wa kurudi kwake kwa ushindi, ataliwasilisha kwake mwenyewe kanisa lenye utukufu, waaminifu wa karne zote, walionunuliwa kwa damu yake, lisilo na waa au kunyanzi, lakini takatifu na lisilo na ila. (Mwa. 12:3; Mtdo. 7:38; Waef. 4:11 – 15; 3:8 – 11; Math. 28:19, 20; 16:13 – 20; 18:18; Waef. 2:19 – 22; 1:22, 23; 5:23 – 27 Wakol. 1:17, 18).

13.               Masalio na Utume Wake

Kanisa la ulimwengu linajumuisha wale wote ambao kwa kweli wanamwamini Kristo, lakini katika siku za mwisho, kipindi cha kuenea kwa ukengeufu, masalio wameitwa kuzishika amri za Mungu na imani ya Yesu. Masalio hawa hutangaza kuwadia kwa saa ya hukumu, hutangaza wokovu kupitia kwa Kristo, na hupiga mbiu ya kukaribia kwa marejeo yake. Tangazo hili huwakilishwa katika mfano wa malaika watatu wa ufunuo 14; huambatana na kazi ya hukumu mbinguni na kuwa na matokeo ya kazi ya toba na matengenezo duniani. Kila muumini anatakiwa kuwa na sehemu binafsi katika ushuhuda huu wa ulimwenguni kote. (Ufun. 12:17; 14:6 – 12; 18:1 – 4; IIWakor. 5:10; Yuda 1:3, 14; IPet. 1:16 – 19; IIPet. 3:10 – 24; Ufun. 21:1 – 14).

14.               Umoja katika Mwili wa Kristo

Kanisa ni mwili mmoja ulio na washiriki wengi, walioitwa kutoka kila taifa, kabila, lugha, na watu. Katika Kristo tu viumbe wapya; ubainishi wa rangi, tamaduni, elimu, na taifa, na tofauti kati ya tabaka ya juu na ya chini, tajiri na masikini, mwanamume na mwanamke, havipaswi kuleta mgawanyiko miongoni mwetu. Sote tu sawa katika Kristo, ambaye kwa Roho mmoja ametufunga katika ushirika mmoja pamoja na yeye na sisi wenyewe kwa wenyewe; tunapaswa kutumika na kutumikiwa pasipo upendeleo au kusita. Kupitia kwa ufunuo wa Yesu Kristo katika Maandiko tunashiriki imani na tumaini moja,, na tunawafikia wote kwa ushuhuda mmoja. Umoja huu una chimbuko lake katika umoja wa Mungu mmoja mwenye nafsi tatu ambaye ametufanya sisi kuwa watoto wake. (Warumi 12:4, 5; IWakor. 12:12 – 14; Math. 28:19, 20; Zab. 133:1; IIWakor. 5:16, 17; Mdo. 17:26, 27; Wag. 3:27, 29; Wakol. 3:10 – 15; Waef. 4:14 – 16; 4:1 – 6; Yoh.17:20 – 23)




15.               Ubatizo

Kwa njia ya ubatizo tunakiri imani yetu katika kifo na ufufuo wa Yesu Kristo, na kushuhudia kufia kwetu dhambi na kusudi letu la kuenenda katika upya wa maisha. Hivyo tunamkubali Kristo kuwa Bwana na Mwokozi, tunakuwa watu wake, na tunapokelewa kama washiriki na kanisa lake. Ubatizo ni mfano wa muungano wetu pamoja na Kristo, msamaha wa dhambi zetu, na kupokea kwetu Roho mtakatifu. Ni kwa kuzamishwa majini na unategemea uthibitisho wa imani katika Yesu na ushahidi wa toba ya dhambi. Unafuatia mafunzo katika Maandiko Matakatifu na ukubali wa mafundisho yake. (Warumi 6:1 – 6; Wakol. 2:1,2,13; Mdo. 16:30 33; 22:16; 2:38; Math. 28:19, 20)

16.               Meza ya Bwana

Meza ya Bwana ni ushirika katika mfano wa mwili na damu ya Yesu kama udhihirisho wa imani katika yeye, Bwana na Mwokozi wetu, katika uzoefu huu wa ushirika Kristo anakuwepo kukutana na kuwaimarisha watu wake. Kadiri tunavyoshiriki, kwa furaha tunatangaza mauti ya Bwana mpaka arudipo tena. Maandalizi kwa ajili ya Meza ya Bwana hujumuisha kujihoji nafsi, toba na ungamo. Bwana aliamuru huduma ya kutawadhana miguu kumaanisha kutakaswa upya, kuonyesha nia ya kutumikiana wenyewe kwa wenyewe katika unyenyekevu ufananao na wa Kristo, na kuungana mioyo yetu katika upendo. Huduma ya meza ya Bwana ni wazi kwa waumini wote Wakristo. (IWakor. 10:16, 17; 11:23 – 30; Math. 26:17 – 30; Ufu. 3:20; Yoh. 6:48 – 63; 13:1 – 17)

17.               Karama za Roho na Huduma

Mungu huwakirimia washirki wote wa kanisa lake katika kila kizazi karama za kiroho ambazo kila mshiriki atatumia katika huduma ya upendo kwa ajili ya mema ya kawaida ya kanisa na ya wanadamu. Zikitolewa kwa wakala wa Roho Mtakatifu, ambaye humgawia kila mshiriki kama apendavyo yeye, karama hizo hutoa uwezo wote na huduma zinazohitajiwa na kanisa katika kutekeleza shughuli zake zilizoamuriwa na Mungu. Kulingana na Maandiko, karama hizi hujumuisha huduma kama imani, uponyaji, unabii, mahubiri, mafundisho, utawala, upatanisho, huruma, na huduma ya kujinyima na ufadhili kwa ajili ya msaada na faraja kwa watu. Baadhi ya washiriki huitwa na Mungu na kukirimiwa na Roho kwa ajili ya shughuli zinazotambuliwa na kanisa katika uchungaji, uinjilisti, utume, na huduma za kufundisha zinazohitajika hasa katika kuwapatia zana washiriki kwa ajili ya huduma, kulijenga kanisa hadi ukomavu wa kiroho, na kukuza umoja wa imani na maarifa ya Mungu. Pale washiriki wanapozitumia karama hizi za kiroho kama mawakili waaminifu wa neema mbali mbali za Mungu, kanisa hulindwa dhidi ya mivuto miharibifu ya mafundisho ya uongo, na hukua kwa ukuaji unaotoka kwa Mungu, na hujengeka imara katika imani na upendo. (Warumi 12:4 – 8; IWakor. 12:9 – 11, 27, 28; Waef. 4:8, 11 – 16; Mdo 6:1 – 7; ITim. 3:1 – 13; IPet. 4:10, 11.)

18.               Karama ya Unabii

Mojawapo ya karama za Roho Mtakatifu ni unabii. Karama hii ni alama – kitambulishi cha kanisa la masalio na ilidhihirishwa katika huduma ya Ellen G White. Kama mjumbe wa Bwana, maandishi yake ni chanzo kiendelezi na yenye mamlaka ya ukweli yanayolipatia kanisa faraja, uongozi, mafundisho, na maonyo. Pia yanaweka wazi kwamba Biblia ndiyo kanuni ambayo kwayo mafundisho yote na uzoefu lazima vipimwe. (Yoeli 2:28, 29; Mdo. 2:14 – 21; Waebr. 1:1 – 3; Ufun. 12:17; 19:10)

19.               Sheria ya Mungu

Kanuni kuu za sheria ya Mungu zimetiwa pamoja katika amri kumi na mfano wake ulidhihirishwa katika maisha ya Kristo. Nazo zinadhihirisha upendo wa Mungu, mapenzi yake, na makusudi yake kuhusu mwenendo wa binadamu na mahusiano nazo ni sharti kwa watu wote katika kila kizazi. Amri hizi ndiyo msingi wa agano la Mungu na watu wake na kanuni katika hukumu ya Mungu. Kupitia uwakala wa Roho Mtakatifu zinasonda dhambi na kuamsha hisia za hitaji la Mwokozi. Wokovu wote ni katika neema, na si kwa matendo, lakini tunda lake ni utii kwa amri kumi. Utii huu hukuza upendo wetu kwa Bwana na wajibu kwa ajili ya wanadamu wenzetu. Utii wa imani hudhihirisha uwezo wa Kristo kubadilisha maisha na hivyo huimarisha ushuhuda wa Kikristo. (Kut. 20:1 – 17; Zab. 40:7, 8; Math. 22:36 – 40; Kumb. 28:1 – 14; Math. 5:17 – 20; Waebr. 8:8 – 10; Yoh. 15:7 – 10; Waef. 2:8 – 10; IYoh. 5:3; Warumi 8:3, 4; Zab. 19:7 – 14).

20.              Sabato

Muumbaji mkarimu, baada ya siku sita za uumbaji, alipumzika siku ya saba na kuanzisha Sabato kwa ajili ya watu wote kama kumbukumbu ya uumbaji. Amri ya nne ya sheria za Mungu zisizobadilika inaagiza adhimisho la Sabato hii ya siku ya saba kama siku ya mapumziko, ibada, na huduma kulingana na mafundisho na uzoefu wa Yesu, Bwana wa Sabato. Sabato ni siku ya mawasiliano yenye furaha pamoja na Mungu na sisi kwa sisi. Ni mfano wa ukombozi wetu katika Kristo, ishara ya utakaso wetu, ishara ya utii wetu, na mwonjo wa umilele wetu wa siku zijazo katika ufalme wa Mungu. Sabato ni ishara ya daima ya Mungu ya agano la milele la Mungu kati yake na watu wake. Utunzaji wa furaha wa wakati huu mtakatifu toka jioni hadi jioni, jua kuchwa hadi jua kuchwa, ni adhimisho la matendo ya Mungu ya uumbaji na ukombozi. (Mwa. 2:1 –3; Lut. 20:8 – 11; Luka 4:16; Isaya 56:5, 6; 58:13, 14; Math. 12:1 – 12; Kut. 31:13 – 17; Ezek. 20:12, 20; Kumb. 5:12 – 15; Waebr. 4:1 – 11; Walawi 23:32; Marko 1:32).

21.               Uwakili

Sisi tu mawakili wa Mungu, tuliokabidhiwa na yeye wakati na fursa, uwezo, na mali, na mibaraka ya dunia na rasilimali zake. Tunawajibika kwake kwa matumizi yake sahihi. Tunakiri umilikaji wa Mungu kwa huduma ya uaminifu kwake na kwa wandadmu wenzetu, na kwa kurudisha zaka na kutoa sadaka kwa ajili ya utangazaji wa injili Yake na kwa utengemezaji na ukuaji wa kanisa lake. Uwakili ni fursa iliyotolewa kwetu na Mungu kwa ajili ya malezi katika upendo na ushindi dhidi ya choyo na tamaa. Wakili hufurahia mibaraka inayowajia wengine kama matokeo ya uaminifu wake. (Mwa. 1:26 – 28; 2:15; INyak 29:14; Hagai 1:3 – 11; Malaki 3:8 – 12; IWakor. 9:9 – 14; Math.23:23; IIWakor. 8:1 – 15; Warumi 15:26, 27).

22.              Mwenendo wa Kikristo

Tumeitwa kuwa watauwa wanaofikiri, kujisikia, na kutenda kulingana na kanuni za mbinguni. Ili Roho aumbe upya ndani yetu tabia ya Bwana wetu tunajihusisha tu katika mambo yale ambayo yatazaa katika maisha yetu usafi unaofanana na Kristo, afya na furaha katika maisha yetu. Hii inamaanisha kwamba maraha na maburudisho yetu yanapaswa kufikia viwango vikuu vya maonji na uzuri wa Kikristo. Huku tukitambua tofauti za kiutamaduni, mavazi yetu yanapaswa yawe ya kawaida, si ya anasa; na safi, yanayostahili wale ambao uzuri wao wa kweli asili yake siyo mapambo ya nje, bali asili yake ni mapambo yasiyoharibika, yenye roho ya upole na utulivu. Pia inamaanisha kwamba kwa kuwa miili yetu ni mahekalu ya Roho Mtakatifu, tunapaswa kuitunza kwa akili yenye afya sana kadiri invyowezekana na kuepuka vyakula vilivyo najisi, vilivyotajwa katika Maandiko Matakatifu. Kwa vile vinywaji vya vileo, tumbaku na maatumizi mabaya ya madawa hudhuru miili yetu, yatupasa kuepukana navyo pia. Badala yake tunapaswa kujishughulisha na cho chote kile kitakacholeta mawazo yetu na miili yetu viwe katika nidhamu ya Kristo, ambaye hutamani uzima wetu, furaha na wema. (Warumi 12:1, 2; IYoh. 7; 2:6; Waef. 5:1 – 21; Wafilipi 4:8; IIWakor. 10:5; 6:14 – 7:1; IPet. 3:1 – 4; IWakor. 6:19, 20; 10:31; Walawi 11:1 – 47; IIIYoh. 2).

23.              Ndoa na Familia

Ndoa ilianzishwa na Mungu katika Edeni na ikathibitishwa na Yesu kuwa muungano wa maisha yote kati ya mwanamume na mwanamke katika wenzi wenye upendo. Kwa Mkristo kifungo cha ndoa ni kwa Mungu na pia kwa mwenzi, na kishirikiwe tu na wenzi wenye imani moja. Upendo wa hiari, heshima, staha, na uwajibikaji ndizo fito za (kujengea) uhusiano huu, ambao utaakisi upendo, utakatifu, ukaribu, uthabiti wa uhusiano kati ya Kristo na kanisa lake. Kuhusu talaka, Yesu alifundisha kwamba mtu anayemwacha mwenzi, isipokuwa kwa sababu ya uasherati, na akaoa (au kuolewa) na mwingine, azini. Ingawa baadhi ya mahusiano ya kifamilia huenda yakashindwa kufikia lengo, wenzi katika ndoa ambao wamejitoa kikamilifu kila mmoja kwa mwenzake katika Kristo wanaweza kufaulu kufikiliza katika umoja wenye upendo kupitia uongozi wa Roho Mtakatifu na malezi ya kanisa. Mungu hubariki familia na anakusudia kwamba washirika wake watasaidiana wao kwa wao kufikia upevu kamili. Wazazi wawalee watoto wao katika kumpenda na kumtii Bwana. Kwa kielelezo chao na maneno yao wawafundishe kwamba Kristo ni mtiishaji mwenye upendo, daima mpole na mwenye kujali, anayetaka wawe viungo vya mwili wake, familia ya Mungu. Kukuza ukaribu wa uhusiano wa kifamilia ni mojawapo ya alama (ya kujulisha) ujumbe wa mwisho wa injili. (Mwa. 2:18 – 25; Math. 19:3 – 9; Yoh. 2:1 – 11; IIWakor. 6:14; Waef. 5:21 – 33; Math. 5:31, 32; Marko 10:11, 12; Luka 16:18; IWakor. 7:10, 11; Kut. 20:12; Waef. 6:1 – 4; Kumb. 6:5 – 9; Mith. 22:6; Malaki 4:5, 6).

24.              Huduma ya Kristo katika Hekalu la Mbinguni

Kuna hekalu mbinguni, hema la kweli lililosimamishwa na Bwana na siyo mwanadamu. Ndani yake Kristo anahudumu kwa niaba yetu, akiwezesha kupatikana kwa ajili ya waumini fanaka za kafara yake ya upatanisho iliyotolewa mara moja msalabani kwa ajili ya wote. Alizinduliwa kuwa Kuhani wetu Mkuu na akaanza huduma yake ya uombezi wakati wa kupaa kwake mbinguni. Mnamo mwaka 1844, mwishoni mwa kipindi cha unabii wa siku 2300, aliingia katika awamu ya pili na ya mwisho ya huduma yake ya upatanisho. Ni kazi ya hukumu ya upelelezi ambayo ni sehemu ya mwisho ambayo hatimaye itakomesha dhambi yote, iliyokuwa mfano wa kutakaswa kwa hekalu la kale la Waebrania katika siku ya upatanisho. Katika huduma hiyo kielelezo hekalu lilitakaswa kwa damu ya wanyama wa kafara, lakini mambo ya mbinguni hutakaswa kwa kafara kamili ya damu ya Yesu. Hukumu ya  upelelezi hufunua kwa viumbe wa mbinguni ni nani miongoni mwa wafu wamelala katika Kristo na hivyo, katika Yeye wanahesabiwa kustahili kuwa na sehemu katika ufufuo wa kwanza. Pia inadhihirisha wazi ni nani miongoni mwa walio hai wanakaa ndani ya Kristo, wakishika amri za Mungu na imani ya Yesu, na katika Yeye, hivyo basi, wako tayari kwa ajili ya kuhamishwa kuingia katika ufalme wake wa milele. Hukumu hii huthibitisha haki ya Mungu katika kuwaokoa wale wanaomwamini Yesu. Hutangaza kwamba wale waliodumu kuwa watiifu kwa Mungu watapokea ufalme. Hitimisho la huduma hii ya Kristo itakuwa ndiyo mwisho wa kufungwa kwa mlango wa rehema ya wanadamu kabla ya marejeao ya Yesu. (Waebr.8:1 – 5; 4:14 – 16; 9:11 – 28; 10:19 – 22; 1:3; 2:16, 17; Dan. 7:9 – 27; 8:13, 14; 9:24 – 27; Hes. 14:34; Ezek. 4:6; Walawi 16; Ufun. 14:6,7; 20:12; 14:12; 22:12).

25.              Kuja kwa Kristo mara ya pili

Kuja kwa Kristo mara ya pili ndilo tumaini lenye baraka la kanisa, hitimisho kuu la injili. Kuja kwa Mwokozi kutakuwa halisi, binafsi, kutakakoonekana, na kwa dunia nzima. Atakaporudi, wenye haki waliokufa watafufuliwa na pamoja na wenye haki walio hai watavikwa utukufu na kuchukuliwa kwenda mbinguni, lakini waovu watakufa. Kutimizwa karibu kabisa kwa sehemu nyingi za unabii pamoja na hali ya sasa ya ulimwengu, huonyesha kwamba kuja kwa Kristo ku karibu sana. Wakati wa tukio hilo hakukufunuliwa, na hivyo basi tunahimizwa kuwa tayari kwa nyakati zote. (Tito 2:13; Waebr. 9:28; Yoh. 14:1 – 3; Mdo. 1:9 – 11; Math. 24:14; Ufun. 1:7; Math. 24:43, 44; IWathes. 1: 7 – 10; 2:8; Ufun. 14:14 – 20; 19:11 – 21; Math. 24; Marko 13; Luka 21; IITim. 3:1 – 5; IWathes. 5:1 – 6).

26.              Mauti na Ufufuo

Mshahara wa dhambi ni mauti. Lakini Mungu, ambaye peke yake hapatwi na mauti, atawapa uzima wa milele waliokombolewa wake. Mpaka siku hiyo mauti ni hali ya kutokuwa na fahamu kwa watu wote. Wakati Kristo, aliye uzima wetu atakapotokea, wenye haki waliofufuliwa na wenye haki walio hai watavikwa utukufu na kunyakuliwa juu ili kumlaki Bwana wao. Ufufuo wa pili ni ufufuo wa waovu, utatokea miaka elfu moja baadaye. (Warumi 6:23; I Tim. 6:15, 15; Mhu. 9:5, 6; Zab. 146:3, 4; Yoh. 11:11 – 14; Wakol. 3:4; IWakor. 15:51 – 54; IWathes. 4:13 – 17; Yoh. 5:28, 29; Ufun. 20:1 – 10)

27.              Milenia (miaka elfu) na mwisho wa dhambi

Milenia ni miaka elfu moja ya utawala wa Kristo pamoja na watakatifu wake mbinguni kati ya ufufuo wa kwanza na wa pili. Wakati huo waovu waliokufa watahukumiwa; dunia itakuwa ukiwa na utupu bila wanadamu wakazi walio hai, lakini ikikaliwa na shetani na malaika zake. Mwishowe Kristo na watakatifu wake na Mji Mtakatifu watashuka duniani kutoka mbinguni. Ndipo waovu waliokufa watafufuliwa, nao pamoja na shetani na malaika zake watauzingira mji; lakini moto kutoka kwa Mungu utawateketeza na kuitakasa dunia. Na hivyo ulimwengu utakuwa huru bila dhambi na wenye dhambi milele. (Ufun. 20; IWakor. 6:2, 3; Yer. 4:23 – 26; Ufun. 21:1 – 5; Malaki 4:1; Ezek. 28:18, 19)

28.              Dunia mpya

Katika dunia mpya, ambamo haki hukaa, Mungu ataweka tayari makao ya milele kwa waliokombolewa na mazingira makamilifu kwa maisha ya milele, upendo, furaha na kujifunza mbele zake. Kwa kuwa hapa Mungu Mwenyewe atakaa pamoja na watu wake, na taabu na mauti vitakuwa vimepita. Pambano kuu litakuwa limemalizika, na dhambi haitakauwako tena. Vitu vyote, vyenye uhai na visivyo na uhai vitatangaza kwamba Mungu ni pendo; naye atatawala milele. Amina. (IIPet. 3:13; Isaya 35; 65:17 – 25; Math. 5:5; Ufun. 21:1 – 7; 22:1 – 5; 11:15).

1 comment:

  1. REDIGONDA CHAULO7 February 2018 at 11:19

    UBARIKIWE MTUMISHI KWA KAZI NZURI

    ReplyDelete

Nakuthamini

ikiwa kuna jambo lolote zuri lenye kuboresha au kufundisha usisite kuwasiliana nami. Blog hii ni kwa ajili yetu wote kutufundisha na kutuelekeza yatupasayo kutenda kwa maana wakati umekaribia ambapo yeye ajae anakuja na wala hatakawia. Nyosha mapito yako,tambua tabia yako kila mtafute Bwana maana anapatikana nawe ukimwita atakuitikia.